19/07/2026
Wanufaika wa mradi wa Dumisha Amani wahamasishwa kuomba zabuni za Serikali
Mkuu wa wilaya ya Kigoma, Dkt. Rashid Chuachua, amewahamasisha wanufaika wa mafunzo ya ufundi kupitia Mradi wa Dumisha Amani chini ya ufadhili wa Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Amani na Maendeleo (UNPDF), Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), China Petroleum Pipeline (CPP) kwa kushirikiana Global Peace Foundation (GPF) Tanzania, kuomba zabuni za Serikali kupitia vikundi watakavyojiunga ili waweze kujitegemea.
Chuachua ametoa wito huo tarehe 18 Julai 2026 katika viwanja vya chuo cha Ufundi Stadi na Huduma cha Mkoa wa Kigoma (chuo cha VETA Kigoma) wakati wa hafla fupi ya kufungwa rasmi kwa mafunzo ya Dumisha Amani yaliyotolewa kwa muda wa majuma mawili chuoni hapo.
“Niwatie shime ninyi mnaohitimu leo kujiunga kwenye vikundi ambavyo vitawafanya msajiliwe na mfahamu namna ya matumizi bora ya mfumo wa Serikali wa ununuzi (NeST) ili muweze kuomba zabuni za Serikali ili na nyinyi muweze kupata fursa za kiuchumi na kujitegemea,” alisema Chuachua.
Aidha kwa upande mwingine Chuachua amewakumbusha vijana hao uwepo wa fursa za mikopo kutiko Serikalini isiyokuwa na riba kwa vikundi lakini pia kwa mtu mmojammoja mwenye ulemavu.
Kwa upande wake Afisa Maradi kutoka UNDP-Tanzania Josephine Sepeku amesema katika vyuo 4 ambavyo vimehusika kutoa mafunzo kupitia mradi wa Dumisha Amani kila chuo kitapatiwa dola 42,000 sawa na shilingi 110,748,120 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha vijana (Youth centre) ili vijana katika maeneo hayo waendelee kunufaika na ujuzi walioupata.
Kwa upande wake Alphoncina Mashana, Afisa Mkuza Mitaala Mwandamizi kutoka VETA Makao Makuu amewataka vijana hao kwenda kutumia kikamlifu ujuzi walioupata aidha kwa kujiajiri, kuajiri wengine au kuajiriwa ikiwa ni pamoja na kudumisha amani katika maeneo yanayowazunguka.
Akitoa taarifa fupi, Mkuu wa Chuo cha VETA Kigoma Mhandisi Paulo Kimenya amesema mafunzo hayo yalianza rasmi tarehe 6 Julai 2026 kwa muda wa wiki mbili yakiwa na jumla ya washiriki 60, wanawake 38 na wanaume 22.
Amesema mafunzo yamehusisha stadi nne ambazo ni Ubunifu, Ushonaji na Teknolojia ya Nguo, Ufundi Bomba, Mapishi na Umeme wa Majumbani
Naye Amina Issa kwa niaba ya wahitimu wenzake amesema mafunzo hayo yamewajengea uwezo wa kutambua fursa za kiuchumi zilizopo katika jamii, kuanzisha shughuli za uzalishaji mali, kufanya kazi kwa ushirikiano kupitia vikundi vya ujasiriamali, pamoja na kujenga utamaduni wa amani, mshikamano na uvumilivu katika jamii yao.
19/07/2026
17/07/2026
17/07/2026
17/07/2026